Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa klabu ya Yanga, Dismas Ten amekosoa wanaosema kuwa John Bocco ndiyo mfungaji bora wa muda wote wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara badala ya Mohammed Hussein Daima (Mmachinga) ambaye ana idadi kubwa ya magoli kuliko Bocco.
Kwa mujibu wa Ten licha ya kukubali ubora wa Bocco kwa umahiri wake akiwa mbele ya lango la timu pinzani, Mmachinga bado ni mfungaji wa muda wote kutokana na kujikusanyia idadi ya mabao 152
“Kuna eneo moja linalipa shaka kidogo,hili la kuitwa mfungaji bora wa muda wote wa ligi kuu ya Tanzania Bara, akiwa na magoli 113 kama sikosei, nadhani hili haliko sawa,” ameandika Ten
“Iko hivi katika miaka 13 aliyocheza ligi kuu Mohamed Hussein Daima alifunga jumla ya magoli 152, so ni vigumu John Bocco aliyeanza kucheza soka la ushindani 2008 kuitwa mfungaji BORA wa muda wote wa ligi kuu!”
Ten ameorodhesha idaidi ya mabao kwa miaka 13 ambayo Mohamed Hussein aliweka kimiani ambapo mwaka 1993 alifunga magoli 13, 1994 magoli 20, mwaka 1995 Magoli 21, mwaka 1996 magoli 14, mwaka 1997 magoli 12, mwaka 1998 magoli 26, mwaka 1999 magoli 11.
Miaka mingine ni mwaka 2000 magoli 13, mwaka 2001 magoli 4, mwaka 2002 magoli 3, mwaka 2003 magoli 5, mwaka 2004 magoli 4, mwaka 2005 magoli 7.
Kwa mujibu wa Ten idadi hiyo ya magoli aliipata alipokuwa akicheza kwenye timu za Bandari Mtwara, Yanga SC, Simba SC, Mbanga Fc Kigoma pamoja na Twiga Kinondoni .
Amesema hakuna kosa lolote kwa Bocco isipokuwa pengine kukosekana kwa kitengo cha kutunzia kumbukumbu ndani ya Shirikisho la Soka Nchini Tanzania (TFF) ndIYo sababu kubwa ya uwepo kwa sintofahamu hizo.
“Yeye anaongoza..! Nani wa pili nani wa tatu..! Labda isemwe kwa kizazi chake kuanzia 2008 alipoanza kucheza soka la ushindani, Bocco mchezaji mzuri, lakini hili la kuitwa mfungaji bora wa muda wote wa ligi kuu Tanzania Bara hili siyo sawa.”